Header Ads

MWALIMU AUAWA KINYAMA, MTOTO WAKE AJERUHIWA

Mwalimu wa Shule ya Msingi Nyakatundu iliyopo Rufiji mkoani Pwani, Rafaela Msemwa ameuawa kwa kukatwa mapanga na watu wasiojulikana usiku wa kuamkia Agosti 6, 2023.

 

Pamoja na kutekeleza unyama huo, watu hao pia walimjeruhi mtoto wake mwenye umri wa miaka minne, aliyejulikana kwa jina la Bravian Mwamwenda na kumsababishia jeraha kubwa usoni na kwa sasa anaendelea na matibabu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.

 

Mpaka sasa Bravian ameendelea kupokea matibabu kutoka kwa wataalamu bingwa na tayari wamemfanyia upasuaji wa jicho na wanasubiri kumfanyia vipimo vingine kuangalia iwapo jicho hilo litaweza kuona tena.

 

Hayo yamesemwa na baba mdogo wa marehemu, Nolasko Msemwa akiwa nyumbani kwao wilayani Ludewa Mkoa wa Njombe kuhusiana na mauaji hayo.

 

Mwili wa Rafaela umesafirishwa kutoka Rufiji kuelekea Dar es Salaam kwa ajili ya kufanya taratibu nyingine za maziko.

 

Akizungumzia suala hilo, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu Rufiji, Protas Mutayoba amekiri kutokea kwa tukio hilo na amesema tayari uchunguzi umeanza ili kuwabaini waliohusika na mauaji hayo.

 

“Tukio limetokea usiku wa Jumamosi kuamkia Jumapili Agosti 6, huyu mama ni mwalimu wa Shule ya Nyakatundu, aliuawa na watu ambao hawajulikani na wakamuumiza mtoto wake mdogo wa miaka minne, kwa hiyo tunaendelea kufuatilia kuona namna ya kuwapata hawa waliotenda kosa hilo,” amesema kamanda huyo.

 

Kwa mujibu wa RPC, Mwalimu Rafaela alikuwa anaishi peke yake na mtoto wake kwenye nyumba ya shule na ni mgeni eneo hilo ametokea Tarime, mkoani Mara.

 

“Kwa mujibu wa Ofisa Elimu wa Wilaya ya Rufiji, tangu amehamia shuleni hapo hajafikisha miezi mitatu,” amesema Kamanda Mutayoba.

 

Akizungumzia namna walivyobaini mauaji hayo, Kamanda Mutayoba amesema ni baada ya mwalimu mwenzake kufika nyumbani hapo akimfuata waende kanisani kama ilivyokuwa miadi yao ya siku ya Jumamosi jioni.

 

“Kuna mwalimu ambaye ni jirani yake, ndiye aliyegundua mauaji hayo. Jioni waliagana kwamba atampitia waende wote kanisani, ilipofika asubuhi akawa anamtafuta ili waende, sasa akawa hapatikani kwenye simu, ikabidi aende nyumbani kwake ndiyo akakutana na hali ile,” amesema kamanda huyo.

 

Amesema kwa upande wa Jeshi la Polisi tayari wameanza msako; “kazi yetu ni lazima tufanikishe kuwakamata na kuwachukulia hatua za kisheria wote waliotenda uovu huu, kama ni mmoja au wengi tupo kazini, tunafanya upelelezi wetu na tutawatia mbaroni tu’’.

 

Kwa upande wa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji, Michael Gwimile amesema Rafaela alikuwa mtumishi wa halmashauri divisheni ya elimu ya awali na msingi.

 

“Halmashauri na menejimenti imepokea kwa masikitiko taarifa za kifo chake na inatoa pole kwa ndugu, jamaa na marafiki,” amesema Gwimile.

 

Msiba wa mwalimu huyo uko nyumbani kwa shemeji yake maeneo ya Ubungo Makoka, jijini Dar es Salaam.

No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.