Header Ads

MKURUGENZI MANISPAA MOROGORO AFUNGIA NYUMBA 14 ZA KULALA WAGENI KWA KOSA LA KUKWEPA KODI ZA SERIKALI.




Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro Sheilla Lukuba amefunga jumla ya nyumba za kulala 14 zilizopo Manispaa baada ya kufanya ukaguzi wa kushitukiza jana tarehe Novemba 16 katika eneo la Msamvu.
Akiwa katika ukaguzi huo Mkurugenzi Sheilla ambaye aliongozana na maafisa kutoka Idara ya fedha na Biashara Manispaa wamebaini kuna udanganyifu mkubwa unaofanywa na wafanyabishara hao kwa kutowaandika katika vitabu wageni wanaofika na kulala katika nyumba hizo na lengo ikiwa ni kukwepa kulipa kodi ya ushuru wa hotel.
"Leo nimeamua kufanya ukaguzi huu kwa mara ya pili,wiki tatu zilizopita nilifanya ukaguzi kama huu na ukaguzi umekuwa ukiendelea katika maeneo mbalimbali na kubwa nilichokibaini ni udanganyifu unaofanywa na wafanyabiashara hawa,na wengi wana vitabu viwili yani cha bosi ambacho kinaandikwa ukweli na kitabu cha Manispaa hakijazwi kabisa ili kukwepa kulipa kodi"Alisema Mkurugenzi Sheilla.
Aidha Mkurugenzi Sheilla amemwagiza Mweka Hazina wa Manispaa Ponceano Kilumbi kuwatoza faini ya Tsh milioni moja kila nyumba ya kulala wageni iliyofungiwa ili iwe fundisho kwa wafanyabishara wote wanaokwepa kulipa kodi na kufanya udanganyifu.
Na kwa upande wa Mweka Hazina Ndg. Kilumbi amehahidi kutekeleza agizo hilo na kueleza kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Fedha ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2015 ya hotel levy inawataka wafanyabiashara hao kuwaorodhesha wageni wote wanaolala katika nyumba hizo katika vitabu vilivyotolewa na Halmashauri ambavyo ukaguliwa na Manispaa kwaajili ya kulipa kodi kulingana na wageni aliowapata katika kipindi husika.
Pia Mkurugenzi Sheilla ametoa wito kwa wafanyabishara wengine wote kuacha kufanya udanganyifu kwa kuwa Serikali iko kazini na haitasita kuwachukulia hatua wale wote wanaofanya udanganyifu ikiwemo na kuwafikisha mahakamani wale wanaokaidi maagizo ya Serikali .
Ukaguzi Huo umehusisha nyumba za kulala wageni 20, na nyumba 14 zilifungiwa kutokana na kufanya udanganyifu na nyumba za kulala wageni 6 zilikutwa hazina makosa na kuelekezwa kuendelea kutii sheria bila shuruti.

No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.