Header Ads

TAS , WADAU WAADHIMISHA KILELE SIKU YA WATU WENYE UALBINO DUNIANI KWA KUGAWA BAADHI YA MAHITAJI KWA WANAFUNZI.

 

Innocent Mkenda, Afisa Mawasiliano TAS, akigawa baadhi ya vitu kwa wanafunzi.

CHAMA Cha Watu wenye Ualbino Mkoa wa Morogoro, (TAS) kwa kushirikiana na wadau mbalimbali katika jamii na vyuo vikuu wamegawa   baadhi ya mahitaji ya shule ikiwamo Madaftari, Soksi, Peni na Penseli pamoja na Pedi kwa   wanafunzi  wanaotoka kwenye familia duni zisizo na uwezo pamoja na watoto yatima Mtaa wa Ruvuma Kata ya Mlimani Manispaa ya Morogoro.

Akizungumza mara baada ya ugawaji wa mahitaji hayo, Mwenyekiti wa TAS Mkoa wa Morogoro, Hassan Mikazi,amesema zoezi hilo la ugawaji wa mahitaji   litakuwa endelevu na awamu hii inahusisha wanafunzi wanaotoka familia zisizo na uwezo ambao wanagawiwa vifaa vya shule  huku wanafunzi wote waaliojitokeza katika zoezi hilo waliweza kupatiwa mahitaji hayo.

Mikazi ,amesema  kuwa lengo kubwa la ugawaji huo wa baadhi ya mahitaji ya wanafunzi katika Mtaa huo, ni  kutoa hamasa kwa wazazi na walezi kuwapeleka watoto wao shule ili wakapate elimu na watoto hao kusoma kwa bidii kwa manufaa yao ya baadaye na taifa kwa jumla pamoja na kuhamasisha kuinua kiwango cha elimu katika Mtaa huo na Manispaa ya Morogoro na Taifa kwa Ujumla.

" Tukiwa tunaelekea kilele cha Siku ya Watu wenye ualbino Duniani itakayofanyika Juni 13/2022 , sisi TAS kwa kushirikiana na wadau tumeona tuwatembelee ndugu zetu kwa kuwapa tulicho nacho, huu ni upendo ambao unatufanya tusibaguane kati ya watu wenye ualbino na wasio na ualbino, tuendele kushirikiana na kuwa pamoja kwani Albino nae ana haki kama ilivyo wengine" Amesema Mikazi.

Aidha, Mikazi amesema, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan,  imedhamiria  kuleta   maendeleo ya kweli katika Taifa ikiwa ni pamoja na kuinua kiwango cha elimu katika shule za msingi na sekondari kwa kutekeleza mpango wa elimu bila malipo.

Miongoni mwa maada zilizotolewa ni pamoja na nini maana ya Ualbino, albino ni nani na watu wanatakiwa kuwachukuliaje katika mitazamo pamoja na maada ya kuwalinda albino dhidi ya mionzi  ya jua na suala zima la elimu ya ukatili wa kijinsia iliyotolewa na Mwakilishi wa Kituo cha Msaada wa Kisheria Morogoro , Chediel Senzighe.

Baadhi ya Mahitaji yaliyogaiwa leo ni, ugawaji wa rosheni za kuzuia mionzi ya jua kwa watoto wenye ualbino,  Madaftari aina ya Msomi, peni, penseli, ufutio, na pedi kwa watoto wakike walianza kupata hedhi na kufautia na zoezi la upandaji wa miti.

Naye, Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Ruvuma Kata ya Mlimani Manispaa ya Morogoro, Festo Anatory, ametoa shukrani kwa TAS na Wadau wote walioshiriki kwa kufika Mtaani kwake na kugawa baadhi ya mahitaji kwa lengo la kusaidia watoto wanaoishi katika mtaa huo.


No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.