Header Ads

DC MSANDO AKABIDHI MCHORO WA KIMKAKATI KWA WANANCHI WA STAR CITY KIEGEA A NA B.

 

MKUU wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Albert Msando, amekabidhi mchoro wa kimkakati wenye lengo la kuujenga Mji wa Kiegea A na B eneo la Star City Manispaa ya Morogoro.

Mchoro huo amekabidhi Julai 14/2022 katika mkutano wake na wananchi wa eneo hilo ikiwa ni maandalizi ya kuupanga mji huo.

Akizungumza na Wananchi hao, DC Msando,amesema kuwa Wananchi wa Star City watembee kifua mbele kwani wanakwenda kumiliki ardhi yao waliyokuwa wakiisubiria kwa muda mrefu kufuatia eneo hilo kuwa na sintofahamu na Mwekezaji.

Pamoja na kukabidhi ramani hiyo, DC Msando, amesema mji huo wameupanga na kuwa mji wenye hadhi ya kipekee ambao utakuwa na huduma zote muhimu za kijamii na kufungua fursa za ajira kwa wananchi wa eneo hilo.

“Tumewaletea huu mchoro, tulianza na upimaji tukiwa na lengo la kila mwananchi aliye na kipande anakuwa na hati yake miliki ili kujiletea maendeleo, niwaombe baada ya kumiliki haya maeneo msiyauze ,yatunzeni kwa ajili ya vizazi vyenu vya baadae ardhi ni hadhina, hata mjini nako kulikuwa kama hivi” Amesema DC Msando.

Naye Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro, Ally Machela, amesema kwa sasa hatua inayofanyika ni kuhakikisha mji huo unachongwa barabara zote kabla hawajatoa maelekezo ya ujenzi wa nyumba kufuatia kukabidhiwa ramani hiyo.

Machela,  amesema kwa sasa Mji unahitaji kupangwa hivyo wananchi lazima wasikilize maelekezo na maagizo ya viongozi badala ya kukiuka maagizo hayo.

Naye , Afisa Mipango Miji Manispaa ya Morogoro, Emeline Kihunrwa, amesema kwa sasa timu ipo kazini kuhakikisha eneo hilo lote lenye ekari 4500 linapimwa na kupangwa ili wananchi waweze kupata hati zao.

Upande wa Mwananchi, Elizabeth Chigua, ameshukuru Uongozi wa Mkoa, Wilaya na Manispaa kwa kuchukua hatua za kuwatambua na kuwamilikisha ardhi baada ya muda mrefu kuitwa wavamizi.

“SENSA KWA MAENDELEO ,JIANDAE KUHESABIWA TAREHE 23/08/2022”    

 

No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.