Header Ads

MANISPAA YA MOROGORO YAZINDUA MASHINDANO UMITASHUMTA.

 

MANISPAA  ya Morogoro imezindua rasmi mashindano ya Umoja wa Michezo na Taaluma kwa Shule za Msingi Tanzania (UMITASHUMTA).

Uzinduzi huo umefanyika Juni 10, 2022 kwenye viwanja vya shule ya Sekondari Lupanga kata ya Kilakala kwa kuwashirikisha wanamichezo kutoka shule zote za Msingi ndani ya Manispaa hiyo na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa vyama vya michezo pamoja na walimu kutoka shule hizo.

Akifungua mashindano hayo ,Justine Mkurya, ambaye ni Mgeni rasmi wa uzinduzi huo akimwakilisha Mkurugenzi wa manispaa ya Morogoro,  amesema kuwa lengo kubwa la mashindano hayo ni kuunda timu kubwa ya halmashauri itakayowezesha kuleta ushindani.

“leo ndio tunafungua rasmi mashindano haya na lengo kubwa la mashindano hayo ni kuunda timu kubwa na bora katika halmashauri yetu kwenye michezo yote kwahiyo ombi langu kwenu, kila mmoja ashiriki kikamilifu katika eneo alilopangiwa ili tuweze kupata timu bora ya Manispaa ambayo itaenda kutuwakilisha vizuri kwenye mashindano ya Mkoa ambayo mwaka huu Kimkoa yatafanyika ndani ya eneo letu hivyo msituangushe” Amesema Mkurya

Aidha,Mkurya, amewaasa walimu waliopewa dhamana ya kuunda timu ya manispaa  kuacha kuchagua wanamichezo kwa upendeleo

“Niwasihi walimu mliopewa dhamana ya kuunda timu ya Manispaa kuacha tabia ya kuchukua wanamichezo kwa upendeleo, undeni timu kadri mwanafunzi mwenyewe anavyoonesha kipaji chake katika michezo, ili tupate timu imara katika fani zote na tuweze kushiriki kimkoa na hata kitaifa” Ameongeza Mkurya.

Pia wanamichezo hao ambao ni wanafunzi kutoka shule mbalimbali za Msingi ndani ya manispaa hiyo  wametakiwa kuhakikisha kwamba wanakuwa na nidhamu na kujituma katika eneo walilopangiwa katika kipindi chote cha michuano hiyo ili wawe miongoni mwa watakao unda timu ya Manispaa badae kimkoa na kufika kitaifa.

Kwa upande wa Afisa Michezo Manispaa ya Morogoro, Asteria Mwang'mbe, amewataka Waalimu wa michezo Manispaa ya Morogoro kutumia michezo ya UMITASHUMTA  kuibua vipaji kupitia hazina ya Vijana wadogo waliopo katika shule za Msingi  wenye uwezo mkubwa katika michezo mbalimbali.


No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.