Header Ads

DIWANI KILONGO AELEZEA MAFANIKIO MAKUBWA NDANI YA MIAKA 3 KATA YA KIHONDA

DIWANI wa Kata yaKihonda, Mhe. Hamis Kilongo, amesema  katika kipindi cha miaka 3 akiwa madarakani Kata ya Kihonda  imekuwa na mafanikio makubwa sana ukilinganisha na kipindi cha nyuma.

Hayo ameyasema Novemba 25/2023 kwenye Mkutano wa hadhara wa wananchi uliofanyika Ofisi ya Kata Mkutano  wenye lengo la kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM 2020-2023 kwa wananchi  akiwa Madarakani.

Mhe.Kilongo ,amesema kuwa katika kipindi cha miaka iliyopita Kata ya Kihonda imebadilika sana hususani katika sekta ya afya, miundombinu, elimu na huduma za Maji pamoja na uimarishaji wa ulinzi na usalama.

Mhe. Kliongo, amesema Kata ya Kihonda ni miongoni mwa Kata ambazo zimenufaika na miradi mikubwa ya Maendeleo ikiwemo miradi ya barabara kupitia mradi wa Tactics , miradi ya madarasa, Bweni la watoto wenye mahitaji  Maalum  pamoja na Ujenzi wa Hospitali ya Manispaa ambayo ni Mkombozi mkubwa wa huduma za afya kwa Wananchi.

"Nampongeza Mama yetu Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan tumepokea Bilioni 2 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ambayo ipo kwenye Kata yangu,  na sasa majengo yote muhimu yamekamilika tunachosubiria ni vifaa vya samani na vifaa tiba ili Hopsitali hiyo ianze  kutoa huduma na kusogeza huduma jirani kwa wananchi ambaao walikuwa wakifuata huduma Hospitali ya Rufaa  lakini nitakuwa mchoyo wa fadhila bila kumshukuru Mbunge wetu wa Jimbo la Morogoro Mjini, Mhe. Dkt. Abdulaaziz Abood, kwani Katika Kata yetu amekuwa na Mchango mkubwa sana hususani katika Sekta ya elimu kupitia fedha zake za mfukoni pamoja na fedha za mfuko wa Jimbo " Amesema Mhe. Kilongo.

Kwenye upande wa elimu Msingi , amesema amekamilisha umaliziaji wa madarasa 2 Shule ya Msingi Kiegea 'A' ujenzi umekamilika kinachosubiriwa ni upauaji wa bati.

Pia, amesema yapo madarasa 2 Shule ya Msingi Kiegea 'A' ambayo yapo hatua ya linta ambapo mpaka sasa shilingi Milioni 8 zimeshatumika fedha kutoka Manispaa ya Morogoro.

Aidha, amesema Kihonda imepokea Milioni 40 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa 2 ya watoto wenye uhitaji pamoja na matundu ya vyoo na ujenzi umekamilika.

Kwenye  upande wa Sekondari, amesema jumla ya milioni 40 zimetumika katika ujenzi wa madarasa 2 Shule ya Sekondari Uluguru.

Pia, amesema  wapo katika hatua ya umaliziaji wa Bweni la watoto wenye mahitaji Maalum Shule ya Msingi Kihonda  ambapo  mpaka sasa Milioni 80 zimeshatumika fedha kutoka Serikali Kuu.

Mhe. Kilongo ,amesema katika kuimarisha ulinzi na usalama,Kata ya Kihonda, kwa kushirikiana na Wenyeviti wa Mitaa pamoja na Chama Tawala CCM wamejipanga kikamilifu kuhakikisha ulinzi unaimarishwa na wananchi wanashiriki kikamilifu katika ulinzi shirikishi.

Kuhusu Ofisi za  mitaa, amesema alivyoingia madarakani Mitaa mingi haikuwa na Ofisi lakini kwa sasa Kila Mtaa una ofisi ambazo zinaendelea kutoa huduma na kusogeza huduma karibu na wananchi ambapo zile kero kubwa kubwa zinazoshindikana katika Mitaa zinaletwa Ofisi ya Kata.

Kuhusu upande wa matundu ya vyoo, Mhe. Kilongo,amesema amekamilisha ujenzi wa matundu 7 ya vyoo Shule ya Msingi Kihonda yenye thamani ya Milioni 67 fedha kutoka Manispaa ya Morogoro na , ujenzi wa madarasa  5 Shule ya Msingi Azimioa A na B a,ambapo Azimio A madarasa 3 na Azimio B madarasa 2 yenye thamani ya Milioni 100 fedha kutoka Serikali Kuu pamoja na ukamilishaji wa madarasa 2 Shule ya Msingi Kiegea 'A' wenye thamani ya milioni 37.

Pia amekamilisha ujenzi wa matundu  12 ya vyoo Shule ya Msingi Azimio B yenye thamani ya milioni 13,200,000.00 fedha kutoka Serikali Kuu na ujenzi wa matundu hayo upo katika hatua ya umaliziaji.

Katika miaka 3 ya Uongozi wake, amekamilisha ujenzi wa sehemu ya kunawia mikono Shule ya Msingi Azimio B ujenzi wenye thamani ya Milioni 13 pamoja na ujenzi wa matundu 9 ya vyoo Shule ya Msingi Azimio A yenye thamani ya Milioni 10.

Amesema Shule ya Msingi Azimio B haikuwa na Jengo la Utawala lakini kwa sasa waalimu wapo kwenye jengo la Kisasa kabisa na wanafanya kazi kwenye mazingira rafiki.

Aidha, amesema Uluguru Sekondari hawakuwa na Jengo la utawala lakini kwa sasa ujenzi upo kwenye hatua ya madirisha ujenzi ambao umetumia 900,000/= fedha kupitia michango ya wananchi na wazazi.

Katika kuona wanafunzi wa Uluguru wanakuwa na majengo ya kutosha ,mpaka sasa madarasa yamekamilika yenye thamani ya milioni 100 fedha kutoka Serikali Kuu.

Mhe. Kilongo,katika kuimarisha huduma za wakina mama wajawazito, tayari ujenzi wa jengo la wakina mama linaendelea lipo kwenye hatua ya umaliziaji ambalo limetumia milioni 60 fedha kutoka Manispaa ya Morogoro .

idha, kuhusu miundombinu ya barabara, Amesema Kata ya Kihonda ni miongoni mwa Kata ambazo zimepitiwa na mradi wa barabara wa Tactics ambapo barabra ya Yespa pamoja na ya Muhimbili zote zinajengwa kwa Kiwango cha Lami.

" Nimshukuru sana Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutupa mradi huu mkubwa wa barabra  ,niombe wananchi tutoe ushirikiano kwa wakandarasi wa mradi na tuwe wa kwanza kulinda vifaa vya wakandarasi wetu ili wafanye kazi yao kwa muda walipangiwa na wakamilishe kwa wakati ili sisi wananchi tuweze kunufaika na huduma hii ambayo tulikuwa tukiisubiria kwa muda mrefu " Ameongeza Kilongo.

Kuhusu TASAF ,amesema Kata yake walengwa wapo na wanaendelea kunufaika na hizi siku mbili tatu walengwa watapatiwa fedha kwani Ofisi ya Mtendaji inaratibu vizuri zoezi la kuhakikisha walengwa wanapewa fedha.

Akizungumzia Vikundi vya Mkopo, Mhe. Kilongo ,  amesema mikopo haijafutwa bali Serikali imesitisha kwa muda ili kuangalia namna bora ya kuboresha mikopo hiyo ya asilimia 10 inayotoka Halmashauri.

Katika hatua nyengine, ameitaka Jamii  kuunga mkono jitihada zinazofanywa na Serikali, wadau na asasi za kiraia katika kupinga vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake na mabinti ili kujenga jamii yenye usawa.

Aidha, Kilongo , amesema Serikali imeweka sera na mikakati ya kupinga vitendo vyote vya ukatili na nguvu zaidi ni kwa jamii kushiriki kwa ukaribu katika kukemea na kuripoti vitendo hivyo.

Mwisho , Kilongo amewataka wananchi kujiunga na mfuko huo wa afya ili kupunguza gharama  za matibabu wanapopata ugonjwa.

"Ugonjwa hauna hodi, niwaombe wananchi CHF ni bima nzuri sana iliyoboreshwa  fika Ofisi ya Kata utapata utaratibu gharama yake ni Shilingi 30,000/= kwa mwaka kwa  watu 6 kwenye Kaya moja" Ameongeza Mhe. Kilongo.

Naye Afisa Tarafa Manispaa ya Morogoro, Winnfred Kipako, amesema  Ukanda wa Lukobe, Mkundi na Kihonda ni ukanda wenye nguvu kazi kubwa ya Manispaa ndio maana Serikali imewekeza miradi mkibwa ya maendeleo.
Kipako, amewataka wananchi kujenga desturi ya kuhudhuria mikutano kwani sehemu pekee ya kupata majibu ya nini Serikali imefanya na inatarajia kukifanya ni kwenye mikutano halili ya Serikali .

Aidha, Kipako, amewahakikishia wananchi wa Kihonda kuwa ulinzi unaendelea kuimairishwa kwani Serikali imejipanga kuhakikisha ukanda wa Lukobe, Mkundi na Kihonda unakuwa na Vituo vya Polisi vya uhakikika katika kusogeza huduma za ulinzi kwa wananchi.

No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.