Header Ads

Mkurugenzi Manispaa Morogoro alitaka Baraza la Wafanyakazi kusimamia misingi ya ushirikishwaji.




MKURUGENZI wa Manispaa ya Morogoro, Sheilla Lukuba, amelitaka Baraza Jipya la Wafanyakazi Manispaa ya Morogoro kuhakikisha wanasimamia mambo yote ya Msingi katika utendaji wa kila siku pamoja na kutetea haki za Wafanyakazi.
Meza kuu ikishauriana jambo katika kikao cha Baraza jipya la Wafanyakazi Manispaa ya Morogoro.
Hayo ameyazungumza leo wakati wa uzinduzi wa Baraza la Wafanyakazi wa Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro lilotiwa saini rasmi na pande zote zinazohusika mnamo tarehe 10, Desemba 2019, katika ukumbi wa Manispaa leo Januari 27, 2020.
Mkurugenzi Manispaa ya Morogoro, Sheilla Lukuba akizindua rasmi Baraza jipya la Wafanyakazi Manispaa ya Morogoro.
Akizungumza na Waandishi wa habari, amesema uzinduzi wa Baraza hilo ni mojawapo ya utekelezaji wa maagizo ya Viongozi wa Serikali yenye lengo la kuwashirikisha wafanyakazi katika Uongozi wa pamoja mahala pa kazi kwa mujibu wa agizo la Mhe. Rais Hayati Julius Kambarage Nyerere tamko namba 1 la mwaka 1970, pamoja na kifungu cha 73, (1) (2), (3) cha Sheria ya ajira na Mahusiano kazini namba 6/2004 na kifungu cha 14 (1) (c) cha Sheria ya Taasisi za Kazi Namba 7/2004.

Amesema Baraza hilo ni chombo kamili kinachosimamia misingi ya ushirikishwaji wa wafanyakazi kuweza kutoa na kupokea ushauri na majadiliano sehemu za kazi kwa maslahi mapana ya Halmshauri ya Manispaa ya Morogoro.

Aidha, amesema majukumu na kazi za Baraza la Wafanyakazi zimeainishwa katika mkataba unaloliongoza Baraza hilo katika kifungu namba.8 ukurasa wa 6 na kifungu namba 10 ukurasa wa 7-8 huku kila pande husika ikiwa na nakala moja kwa ajili ya kufanya rejea ya Mkataba pale inapohitajika kufanya hivyo.

"Tumefungua Baraza letu jipya la wafanyakazi, natoa rai kuwa ili Baraza liweze kusimama vema maslahi na stahili za watumishi ziboreshwe vizuri, lakini Baraza hili linawajibu wa kuishauri Manispaa juu ya vyanzo vipya vya mapato na namna bora ya ukusanyaji mapato, sambamba na kushauriana na mwajiri juu ya ufanisi wa kazi na hatua zinazofaa kuchukuliwa ili kuhakikisha kuwa huduma zitolewazo na wafanyakazi zinaridhisha na zimo katika malengo ya Halmshauri ya Manispaa ya Morogoro na Taifa kwa ujumla" Amesema Sheilla.

Aidha, amewaambia Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi kuwa wanapokuwa kwenye vikao vya baraza wajumbe wote wanahaki sawa  ya kuchangia na kutoa mawazo ya kuboresha Halmashauri katika nyanja zote muhimu hivyo amewataka Viongozi na Wajumbe kuhakikisha wanatoa ushauri wa uboreshaji bila kuogopa wakuu wao wa kazi (katika marejeo ya kifungu Namba 11.0 ukurasa . Namba 8 cha mkataba wa Barza la Wafanyakazi)

Katibu mpya wa Baraza la Wafanyakazi Manispaa ya Morogoro, Feliciana Katemana.

Pia amesema wao ni wawakilishi tu hivyo lazima watambue kwamba wapo wenzao ambao kwa sasa wanafikia takribani 4,293, hivyoi wanatakiwa kuishauri vyema Halmashauri ya Manispaa kwa manufaa ya wenzao ambao hawapo katika kikao hicho.
Katibu Msaidizi mpya wa Baraza jipya la Wafanyakazi
 Manispaa ya Morogoro, Shabani Duru.
Amewashukuru Wajumbe wa Mkutano wote kwa usikivu na kuwatakia majadiliano yenye tija kila mara wanapokutana katika Vikao vyao vya Baraza .

Mwisho amewataka kila mtumishi na Viongozi wa Serikali kuhakikisha wanamsaidia ,Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kufanya kazi kwa mujibu wa Taratibu, Kanuni na Sheria kwa maslahi mapana ya Nchi.

Katika hatua nyengine, kulifanyika uchaguzi wa viongozi wapya wa Baraza la jipya la Wafanyakazi Manispaa Morogoro ambapo aliyeibuka mshindi kwa upande wa Katibu ni Feliciana Katemana aliyepata kura 34 na kufuatiwa na Shabani Duru kwa kura 14 ambaye kura hazikutosha.






   


No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.