Header Ads

WANAFUNZI 640 KUCHAGULIWA KWA UFADHILI WA SAMIA SCHOLARSHIP


WANAFUNZI wenye ufaulu wa juu katika masomo ya sayansi na

hisabati wana nafasi ya kupata ufadhili wa asilimia 100 kwa masomo ya elimu ya juu kupitia mpango wa Samia Scholarship unaotarajiwa kuanza mwaka wa masomo 2023/24.

Mpango huo ulioanzishwa na Rais Samia Suluhu Hassan mwaka 2022 unalenga kuongeza idadi ya wanasayansi nchini ambao watachangia katika maendeleo ya taifa.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda amesema kuwa wanafunzi 640 watachaguliwa kwa ufadhili huo kwa kuzingatia vigezo vya ufaulu, tahasusi na programu za masomo.

“Samia Scholarship ni fursa kubwa kwa wanafunzi wetu wenye vipaji katika sayansi na hisabati. Tunawasihi watumie fursa hii kujipatia elimu bora na kujiandaa kuchangia katika ujenzi wa taifa letu,” amesema Prof. Mkenda.

 Ufadhili huo utagharamia ada ya mafunzo, posho ya chakula na malazi, vitabu na viandikwa, utafiti, bima ya afya, mahitaji maalum ya vitivo, mafunzo kwa vitendo na vifaa saidizi kwa wanafunzi wenye mahitaji maalumu.

Maombi ya ufadhili huo yatawasilishwa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu kwa njia ya mtandao kupitia mfumo wa https://olas.heslb.go.tz kuanzia Jumatatu, Septemba 25, 2023 na orodha ya majina ya wanafunzi wenye sifa za kuomba itapatikana kupitia www.moe.go.tz na www.heslb.go.tz kuanzia wiki ya kwanza ya mwezi Agosti, 2023.

Ameongezea kwa kusema kuwa wanufaika wa ufadhili huo watapaswa kusoma, kuelewa na kusaini mkataba wa makubaliano ya ufadhili wa masomo kati yao na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Wanufaika hao hawataruhusiwa kubadilisha programu za masomo waliyopatiwa ufadhili bila idhini ya maandishi kutoka Wizara hiyo, na pia hawataruhusiwa kuahirisha masomo isipokuwa kwa sababu za kiafya zinazothibitishwa na chuo husika.

Prof. Mkenda ametoa wito kwa wanafunzi wenye sifa za kuomba ufadhili huo kutumia fursa hiyo adhimu na kujiandaa vizuri kwa ajili ya masomo yao.

“Samia Scholarship ni zawadi kutoka kwa Rais wetu mpendwa Samia Suluhu Hassan. Tunamshukuru sana kwa moyo wake wa uzalendo na upendo. Tunawaomba wanafunzi wetu wawe wazalendo pia na kutumia vizuri fursa hii,” amesema Prof. Mkenda.

No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.