Header Ads

KAMATI ZA HUDUMA ZA UCHUMI , ELIMU NA AFYA MANISPAA YA MOROGORO YARIDHISHWA NA UTEKELEZAJI WA MIRADI YA BOOST.


KAMATI ya Huduma za Huduma za Uchumi, Elimu na Afya Manispaa ya Morogoro imeridhishwa na utekelezaji wa ujenzi wa miradi ya shule mpya za Msingi  na Madarasa na vyoo  iliyojengwa na fedha kutoka Serikali Kuu kupitia   mradi wa kuboresha upatikanaji wa fursa sawa  katika ujifunzaji bora wa elimu ya awali na Msingi Tanzania Bara (BOOST) ambayo miradi hiyo ipo katika hatua ya Ukamilishaji.

Pongezi hizo zimetolewa na Kamati hiyo katika ziara ya kukagua miradi ya madarasa na Shule Mpya za Msingi zinazotekelezwa kupitia mradi wa Boost Julai 17/2023.

Miongoni mwa miradi hiyo ambayo Kamati imekagua ni ujenzi wa Shule Mpya ya Msingi Mgaza Kata ya Mindu, ujenzi wa darasa la Elimu Maalum Shule ya Msingi Mazimbu 'A' pamoja na Shule mpya ya Msingi Kata ya Mafisa.

Kamati hiyo ambayo ipo chini ya Mwenyekiti wake Diwani wa Kata ya Kingo, Mhe. Amini Tunda, imepongeza  juhudi zinazofanywa kwa usimamizi wa Kamati za Shule kwani kasi ni nzuri na wanaimani miradi hiyo kwa jinsi inavyokwenda itakamilika vizuri na kutoa elimu kwa watoto.

Aidha , Kamati hiyo imewataka Walimu kuhakikisha wanaboresha Mazingira ya shule kwa kupanda miti ya vivuri, pamoja na maua ili kuweka mazingira safi na kuachana na kutumia fagio mara kwa mara kwa ajili ya kufagia  mazingira badala yake waweke bustani ya maua.

"Kwa niaba ya Kamati hii kwanza tunamshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutupatia fedha hii ya Boost, lakini nimpongeze Mkurugenzi wetu wa Manispaa kwa usimamizi wa miradi hii bila kusahau Kamati za Shule ambazo zimekuwa karibu na ujenzi wa miradi , tunataka sasa wataalamu kuendelea kuwasimamia mafundi ili waweze  kukamilisha ujenzi kwa wakati ili majengo hayo yaweze kutumika na wanafunzi" Amesema Mhe. Tunda.

Katika hatua nyengine, Kamati hiyo, imewataka viongozi wa Serikali za Mitaa kuwashirikisha wananchi wakati wa utekelezaji wa miradi ili kujenga ushirikiano  katika kulinda mazingira pamoja na miundombinu ya shule.

Naye Mjumbe wa Kamati hiyo, Diwani wa Kata ya Uwanja wa Taifa, Mhe. Rashid Matesa, ametoa shukrani  kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan, ambapo amesema  mara baada ya kukamilika kwa ujenzi wa madarasa hayo yataondoa changamoto ya mlundikano wa Wanafunzi  darasani.

Kaimu Mkurugenzi Manispaa ya Morogoro, Jeremia Lubeleje, amesema timu ya wataalamu Manispaa ya Morogoro imejipanga kwa dhati kuhakikisha miradi yote inakamilika kwa wakati licha ya baadhi ya madarasa tayari yamekamilika kwa asilimia 100 na yapo tayari kwa kutumika.

"Kazi inaendelea na sisi Menejimenti ya Manispaa tupo karibu sana na ujenzi wa miradi hii, yapo madarasa yanaendelea na shule mpya zinaendelea na hatua ni nzuri lakini darasa la Elimu Maalum Shule ya Msingi Mazimbu 'A' limekamilika likiwa na viti, meza pamoja na matundu 3 ya Vyoo ,tutahakikisha madarasa yanakamilika  kwa wakati ili yaweze kutoa huduma " Amesema Lubeleje.

JIUNGE NASI , BONYEZA HAPA http://www.chombohurumedia .blogspot.com ku-install App ya chombohurumedia,  bila ya kuingia website

Tweet@chombo huru media,Youtube@chombo huru media, Facebook@chombo huru media, Instagram @chombohuru­­_media

SUBSCRIBE YOUTUBE CHANNEL: chombo huru media.


No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.