Header Ads

DC MSULWA AWATAKA WASOMI NA WAHITIMU VYUO VIKUU KUWA WABUNIFU, KUTUMIA TAALUMA ZAO KUJIAJIRI

 

Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Bakari Msulwa, akizungumza na Wanafunzi wa Vyuo Vikuu vilivyopo Manispaa ya Morogoro  leo Januari 11/2021 katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro. 

Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Christine Ishengoma, akizungumza na  Wanafunzi wa Vyuo Vikuu vilivyopo Manispaa ya Morogoro  leo Januari 11/2021 katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro. 

Mkurugenzi Manispaa ya Morogoro, Sheilla Lukuba, akisikiliza kwa makini Semina iliyokuwa ikitolewa na Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Bakari Msulwa ,  kwa baadhi ya Wanafunzi wa Vyuo Vikuu vilivyopo Manispaa ya Morogoro.

Afisa Mapato Manispaa ya Morogoro, Muksini Mhina,  akizungumza na  Wanafunzi wa Vyuo Vikuu vilivyopo Manispaa ya Morogoro  leo Januari 11/2021 katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro. 

              
               

MKUU wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Bakari Msulwa, amewataka na kuwahimiza Wanafunzi wa vyuo vikuu kutumia taaluma zao katika kubuni mbinu za kujiajiri kwa lengo la kujikwamua na umaskini na kuondokana na utegemezi wa ajira serikalini.

Hayo ameyazungumza katika Kikao na Baadhi ya Wahitimu na wanaoendelea na masomo wa Vyuo Vikuu  tofauti tofauti vilivyopo Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro leo Januari 11,2021.

Akizungumza na Wanafunzi hao, DC Msulwa, amesema  kuwa kumekuwa na upungufu mkumbwa wa ajira serikalini, huku wahitimu wakiendelea kuongeza kila mwaka.  

“Niwaombe na kuwashauri wahitimu wa vyuo vikuu nchini kutumia elimu na ujuzi wanaopata  kujiajiri wenyewe badala ya kusubiri ajira serikalini, Serikali imekuja na mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri hivyo kwa kupitia mikopo hiuo wakikaa vikundi wataweza kufanya mambo makubwa tofauti na ajira ya Serikalini, lakini pia wanafunzi wa vyuo vikuu wakiitumia ipasavyo elimu walionayo itasaidi kuleta maendeleo ya kiuchumi” Amesema DC Msulwa.

DC Msulwa,  amesema baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakikaa mitaani baada masomo yao ya vyuo na ya mafunzo walioyapata jambo ambalo husababisha kushindwa kutimiza malengo yao na kupelekea wimbi kubwa la vijana wasiokuwa na ajira.

Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Christine Ishengoma, amewataka Wanavyuo hao wanaokopeshwa mikopo  kuzingatia utaratibu na sheria ya fedha ya mwaka 2019 inayoratibu zoezi la utoaji wa mikopo kwa vikundi kwa kuhakikisha wanatumia fedha zinazotolewa kwa kufanyia shughuli za kiuchumi zenye tija kwao na zenye kuwawezesha kurejesha mikopo hiyo bila vikwazo na kwa wakati.

 

“Kazi ya serikali ni kuwawezesha wananchi wake kuishi katika muelekeo sahihi na kupata nafuu ya maisha,mikopo hii ni zoezi endelevu hivyo ni lazima irejeshwe .Leo mmeitwa hapa kwa ajili ya kupatiwa elimu ya mikopo hiyo katika kujiajiri na kukumbushwa  sheria na taratibu za fedha hizi, nyie  ni wawakilishi wa wenzenu , tunategemea , elimu hii tunayowapatia hapa iwafikie na wenzenu  wote.”Amesema Mhe. Ishengoma.

Naye, Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro, Sheilla Lukuba, amesema kuwa watahakikisha wanatekeleza agizo la Mhe. Polepole, la Vijana wa vyuo kupatiwa mkopo , huku akiwataka Vijana hao kuhakikisha kuwa mara baada ya kupata mkopo, wanazingatia  sheria  na taratibu za fedha zinazotolewa na Halmashauri baada kutenga asilimia kumi ya mapato yake ya ndani wakati wa  zoezi la utoaji na urejeshaji wa mikopo.

Kwa upande wa , Afisa Maendeleo ya Jamii Manispaa ya Morogoro, Enedy Mwanakatwe, amewataka wanafunzi hao mara baada ya kuanzisha Vikundi na kupatiwa mikopo wahakikishe wanazingatia  utaratibu na sheria ya fedha inayoratibu zoezi la utoaji wa mikopo kwa vikundi kwa kuhakikisha wanatumia fedha zinazotolewa kwa kufanyia shughuli za kiuchumi zenye tija kwao na zenye kuwawezesha kurejesha mikopo hiyo bila vikwazo na kwa wakati.

Kwa upande wa mwakilishi wa Wanafunzi hao, ambaye pia ni Mwenyekiti wa UVCCM Tawi la Chuo Kikuu cha Sokoine-SUA ,Eliya Nyonga Janikila, amemshukuru Mkuu wa Wilaya, Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Ishengoma pamoja na Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro kwa kikao na semina nzuri yenye kufanya Wanafunzi waweze kujiamini katika kutimiza malengo yao pamoja na kutumia vizuri taaluma zao shuleni.

 






No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.