Header Ads

DC CHONJO ATOA MASAA 24 KWA WATENDAJI AMBAO HAWAJAWASIRISHA FEDHA ZA VITAMBULISHO VYA WAJASIRIAMALI KUFIKISHWA MAHAKAMANI



MKUU wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Regina Chonjo, ametoa masaa 24 kwa Watendaji wote ambao hawajawasirisha pesa za Vitambulisho vya Wajasiriamali vilivyotolewa na Mhe.Rais  Dkt.John Magufuli  kufikishwa mahakamani pamoja na kuchukuliwa hatua kali za kinidhamu.
Akizungumza na Waandishi wa Habari leo Desemba 16, 2019, Ofisini kwake, amesema awali watendaji  wa kata walikuwa wanadaiwa Jumla  ya Shilingi Milioni 10,440,000/=  lakini baada ya kuanza ufuatiliaji  na kuwaweka  ndani walirudisha na kubakiza  Shilingi Milioni 5,510,000/=.ambazo hazijawasilishwa hadi leo.
DC Chonjo amesema kuwa, Manispaa ya Morogoro ilipokea jumla ya Vitambulisho  14,146 kutoka katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, ambapo kwa kata zote 29 kila Mtendaji aligawiwa, hivyo katika marejesho ni watendaji 3 (watatu) ndio hawakurejesha pesa hizo aidha kwa njia ya TRA wala ngazi ya   Manispaa.
Amesema kuwa hadi kufikia tarehe 16 Desemba 2019, jumla ya Vitambulisho 12636 vyenye thamani ya Shilingi milioni 257,741,000/= viliuzwa kwa Wajasiriamali ambapo Vitambulisho 275.5 vyenye thamani ya Shilingi Milioni 5,510,000/= fedha zake bado hazijawasilishwa .
Miongoni mwa  Watendaji ambao hawajarejesha pesa hizo ni pamoja na Godfrey Maumba  mtendaji wa kata ya Kichangani ambae anadaiwa Vitambulisho 154 anayedaiwa Shilingi Milioni 3,080,000/=, Maxmilian Makota Mtendaji Kata ya Mbuyuni alichukua Vitambulisho 113.5 anadaiwa Milioni 2,270,000/= na Cecilia Kolukwi Vitambulisho 8 anadaiwa Shilingi 160,000/=.
"Vitambulisho vyote tulivyowagawia  vilionekana vimeuzwa na pesa wametafuna,  Tumejitahidi kuwaita wahusika lakini bado pesa hizo mpaka sasa hawajazirejesha, Afisa utumishi nakuomba hawa watu baada ya kurudisha hizi pesa wachukuliwe hatua kali za kinidhamu, Mhe. Rais ametoa vitambulisho hivi kwa nia njema pamoja na kuwapa heshima Wajasiriamali na kuongeza pato la Taifa sio fedha kuliwa kiholela , nataka mpaka kesho saa 4:00 Asubuhi pesa hizo ziwe zimewasilishwa TRA la sivyo wafikishwe mahakamani haraka sana" Amesema DC Chonjo.
Mbali na Manispaa ya Morogoro, amemuagiza Mkurugenzi wa Halmsahuri ya Morogoro Vijijini kuhakikisha pesa zote za vitambulisho zimepelekwa TRA na wale ambao bado hawajarejesha pesa hizo kwa kuzitumia kwa matumizi yao binafsi watafikishwa Mahakamani na kuchukuliwa hatua  za kinidhamu baada ya kurejesha pesa hizo.
Kwa upand

e wa Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro, Sheilla Lukuba, amesema amepokea agizo la Mkuu wa Wilaya hivyo wanakwenda kulifanyia kazi ili kuhakikisha wale waliokula pesa za Vitambulisho wanafikishwa Mahakamani haraka iwezekavyo.
Amesema Awamu ya Tano chini ya Mhe. Rais Dkt. John Magufuli imedhamiria kuleta mabadiliko hivyo amewataka Watendaji waachane na tabia ya kufanya kazi kwa mazoea badala yake wajikite katika kutoa huduma bora ikiwamo kuzingatia miiko ya kazi na uadilifu kazini.
"Watendaji wasio wazalendo na nidhamu katika nchi hii kiukweli hawatufai tunataka watendaji wenye moyo wa kizalendo, waadilifu na waaminifu kwa ajili ya kulitumikia Taifa kwa ajili ya kuwaletea Wananchi maendeleo nasiyo wao wajilimbikizie mali na kunufaisha matumbo yao, tunahitaji matokeo chanya, Rais wetu Mhe. Dkt John Magufuli ameonesha dhamira ya dhati ya kuwakwamua Wajasiriamali hivyo lazima nasisi tuwe na huruma ya kumsadia kutimiza adhima yake katika kuelekea uchumi wa kati wa Tanzania ya Viwanda" Amesema Sheilla
Ametoa wito kwa Watumishi wote, ikiwamo Wakuu wa Idara, Watendaji wa Kata pamoja  na wa Mitaa waweke uzalendo mbele hususani katika masuala mazima ya maendeleo na mipango mikubwa ambayo Mhe. Rais anaidhamiria kwa Wananchi wake.

No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.