Header Ads

DC MSULWA AWATAKA MADIWANI KUSHIRIKIANA NA WANANCHI KULETA MAENDELEO


Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Bakari Msulwa.

MADIWANI wa Halmashauri  ya Manispaa ya Morogoro wametakiwa kushirikiana na Wananchi pamoja na Watumishi ili kuhakikisha maendeleo katika Kata zao na Halmashauri kwa ujumla.

Akizungumza na Waandishi wa habari, DC Msulwa, amesema kuwa ushirkiano ni chanzo cha mafanikio katika maeneo yoyote hivyo ili kuleta maendeleo katika kipindi hiki cha miaka mitano suala la ushirikiano linatakiwa kupewa kipaumbele .

DC Msulwa, amesema kuwa , Madiwani peke yao hawawezi kutimiza suala la Maendeleo ndio maana Serikali iliweka watumishi katika Halmashauri ili watoe ushirikiano katika kusimamia maendeleo.

Amewataka Madiwani kuhakikisha wanakwenda kusimamia shughuli zote ambazo zinaingiza kipato cha Halmashauri na kuwa mstari wa mbele kupambana katika ukusanyaji wa mapato katika vyanzo vyao ili kuianya Manispaa kutokuwa tegemezi wa Serikali kuu.

“ Wananchi waliwaamini ndio maana waliwachagua , hivyo ninaimani watatoa ushirikiano wa hali ya juu kwenu katika kutekeleza masuala ya Kimaendeleo, cha msingi kuwa na Umoja baina yenu, Madiwani, Watumishi wa Halmashauri  na Wananchi “ Amesema DC Msulwa.

Kwa upande wa Mstahiki Meya wa Manispaa ya Morogoro, Mhe. Pascal Kihanga, amesema ili kuleta maendeleo katika Halmashauri , Madiwani wanatakiwa kuweka kando tofauti zao ili kufanya kazi kwa pamoja na kuangalia maslahi ya Wananchi badala ya kuangalia maslahi ya mtu mmoja mmoja.

“Hii Halmashauri ni yetu, tukishindwa kuiendeleza tutazomewa na wale tuliowashinda na katika uchaguzi ujao Wananchi hawatatuamini tena, mimi kama Meya wenu nitasimamia sheria na nitatoa ushirikiano kwa kila Diwani,  niwaombe tujenge ushirikiano baina ya madiwani , watumishi wa Halmashauri, Wakuu wa Idara pamoja na Wananchi ambapo kwa kufanya hivyo tutaleta chachu ya maendeleo” Amesema Mhe. Kihanga.

No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.