Header Ads

RC Sanare aridhishwa na mwitikio wa Wananchi uandikishwaji Daftari la kudumu la Wapiga Kura.


Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Loata Sanare akionesha Kitambulisho chake mara baada ya kujiandikisha katika Daftari la kudumu la mpiga kura leo katika kituo cha Liti Kata ya Mlimani Manispaa ya Morogoro.
Mhe. Loata Sanare, akisaini katika wakati wa zoezi la kujiandikisha .
Mhe. Loata Sanare, akikagua kwa umakini Majina yake kwa BVR .(kushoto) I.T wa Manispaa Mr Kitutu Mshana.
Mhe. RC Loata Sanare, akielekezana jambo na Afisa Mwandikishaji Jimbo la Morogoro Mjini, Sheilla Lukuba.


Mhe. Loata Sanare, akisalimiana na Wananchi waliojitokeza kujiandikisha .

Mhe. Loata Sanare, akipata maelekezo kutoka kwa Mwandishi msaidizi .


MKUU wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Loata Sanare, amefurahishwa na idadi ya watu wanaoendelea kujitokeza  kujiandikisha katika vituo mbalimbali vya Uandikishaji wa Daftari la kudumu la wapiga katika Jimbo la Morogoro Mjini lilopo Halmshauri ya  Manispaa ya Morogoro.

Akizungumza na Waandishi wa habari leo Februari 06,2020 mara baada ya kujiandikisha katika Kituo cha Liti Kata ya Mlimani, amempongeza Afisa Mwandikishaji wa Jimbo, Waandikishaji wasaidizi pamoja na wote wanahusika katika zoezi hilo kwa hamasa wanayoitoa jambo ambalo linaleta faraja kubwa katika Mkoa wa Morogoro japo kunatakiwa kuongezwa kasi ya uhamasishaji .

RC Sanare ametumia fursa hiyo kuwasisitiza vijana na wale wanaorekebisha taarifa zao kwamba hakuna mtu atakayeruhusiwa kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020 kama hajajiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ama hana kadi ya mpiga kura.

 Hata hivyo, RC Sanare, amewahimiza  vijana waliotimiza miaka 18 na wale ambao mwaka huu mwezi Oktoba wanatarajia kufikisha umri huo wa miaka 18  wajitokeze kwa wingi kujiandikisha ili kutimiza haki yao ya kuwachagua viongozi wanaowataka katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020. 

“Nitoe rai kwa vijana wote wa Kitanzania waliotimiza umri wa miaka 18 au wale ambao watatimiza umri huo ifikapo Oktoba, 2020 wajitokeze kwa wingi na kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura. Hawa ndio walengwa wakuu kwa sababu wanaingia kwa mara ya kwanza katika uchaguzi,ikumbukwe kwamba, bila kujiandikisha hawataweza kutumia haki yao ya msingi ya kuchagua viongozi wanaowataka, hivyo  kujiandikisha kwao kutawahakikishia ushiriki wao katika uchaguzi wa viongozi "Amesema RC Sanare.

Amesema watakaohusika awamu hii ni wapiga kura waliotimiza miaka 18 hivi karibuni, wale watakaotimiza miaka 18 wakati wa Uchaguzi Mkuu Oktoba 2020, waliohama kata au jimbo na kuhamia maeneo mengine ya kiuchaguzi.

Wengine ni waliopoteza kadi au kadi zao kuharibika, wanaohitaji kurekebisha taarifa zao mfano majina ambayo hapo awali yalikuwa yamekosewa sambamba na kuwaondoa wapiga kura waliopoteza sifa kama vile kufariki.

Zoezi hilo la Uboreshaji wa Daftari la kudumu la wapiga kura,  linafanyika kwa mara ya kwanza tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 ambapo llitafanyika nchi nzima na linatarajiwa kukamilika Machi, 2020.

Amesema ana imani kuwa wananchi wakipata elimu kuhusu uboreshaji kama inavyoendelea kutolewa, basi watahamasika kutumia haki yao ya kikatiba ya kujiandikisha katika daftari hilo na hatimaye kushiriki katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020.

Amewataka wananchi wa jimbo hilo kujitokeza kwa wingi kujiandikisha katika daftari la kudumu  la wapiga kura ambayo itawapa  fursa ya kuwachagua viongozi wanaowataka katika uchaguzi mkuu unaotarajia kufanyika ockoba mwaka huu.

1 comment:

  1. Sheila Lukuba ni mkurugenzi wa manispaa ya Morogoro sio afisa mwandikishaji

    ReplyDelete

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.