Header Ads

BODABODA MANISPAA MOROGORO WATOA TAMKO KALI MADEREVA WATAKAO JIHUSISHA NA MAANDAMANO.

 

Uongozi wa CHAWAPIMAMO, ukiwa katika picha ya pamoja Ofisini kwao mara baada ya mahojiano juu ya kupiga vikali maandamano kwa Vijana wa Bodaboda wanaotaka kutumiwa na baadhi ya Vyama vya Siasa kuvuruga amani.

Viongozi wa CHAWAPIMAMO, (kushoto) Katibu wa Chama hicho, Juma Bega, (kulia), Mwenyekiti wa Chama hicho, Justine Mkoba,  wakitoa  ufafanuzi kwa waandishi ambao hawapo pichani kupinga na kulaani maandamano ya vijana ambao wanataka kutumika kuvuruga amani.

CHAMA Cha Waendesha Pikipiki  Manispaa ya Morogoro (CHAWAPIMAMO) ,kimelaani  na kupinga vikali maandamano ya Madereva watakaotumika kufanya maandamano na kuvuruga amani ya nchi.

Akitoa  tamko  kwa  niaba ya  Chama hicho, leo Novemba 03,2020 kwenye Ofisi za Chama hicho kilichopo Kata ya Mji Mpya TTCL Manispaa ya Morogoro  , Mwenyekiti CHAWAPIMAMO, Justine Mkoba, amesema  umoja wao  umepinga njama  zinazofanywa  na  baadhi ya  vyama vya Siasa   ya kuwatumia madereva  hao na kusisitiza kuwa njama hizo hazitafanikiwa katika Manispaa hiyo.

Amesema kinachotaka kufanyika sasa baada ya  uchaguzi kukamilika na matokeo  kutangazwa  kwa kufuata taratibu zote za uchaguzi na Mamlaka halali ni  vurugu na uvunjifu wa amani jambo ambalo amesema halikubaliki badala  yake amewasihi wananchi wafanye kazi  ili  kuiletea nchi yetu maendeleo  zaidi katika awamu ya sasa.

“Tumejipanga kukabiliana na uhuni wowote ambao umepangwa kufanywa kwenye kipindi  hiki na baadhi ya wahuni wachache wasioitakia mema  nchi yetu, tunaomba  vyombo  vya ulinzi visimamie hili kikamilifu na sisi tupo nyuma yao, yule ambaye atafanya maandamano hayo na tukagundua ni mwanachama wetu tutamfuta Uanachama na atachukuliwa hatua kali za sheria ” Amesema Mkoba.

Amemwomba Mhe. Rais, John Pombe Joseph Magufuli,  kuendelea kuiletea maendeleo Tanzania ili itoke kwenye Uchumi wa Kati  hadi Uchumi wa juu kabisa  na hatimaye  kuboresha maisha  ya watanzania wote.

Kwa upande wa Katibu wa CHAWAPIMAMO, Juma Bega, amewaonya madereva wa  Bodaboda ambao kwa namna moja au nyingine  watatumika katika kuvunja Sheria za nchi kwa kupanga  njama za kufanya maandamano  yasiyo ya amani ambayo hayana kibali kutoka Jeshi la Polisi.

Bega, ameongeza kuwa wananchi wameamua kuwachagua viongozi wanao wapenda hivyo hakuna sababu ya watu kuandaa njama za kupinga matokeo ya uchaguzi.

Naye Naibu Katibu wa Chama hicho, Nurani Ismail, ameipongeza Serikali kwa kufanikisha Uchaguzi Mkuu wa Mwaka huu kwa uwazi  ambao umeweza kufuata taratibu zote na kutoa matokeo  kwa wakati.

Kwa mujibu wa Tume ya Uchaguzi Nchini (NEC), Rais mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa John Pombe Joseph Magufuli anatarajiwa kuapishwa Novemba 5 Mwaka huu kwenye uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma.

 

 

No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.