WAKUU WA SHULE , WENYEVITI WA BODI NA MAAFISA ELIMU KATA WATAKIWA KUINUA UFAULU SHULENI
WAKUU wa Shule za Sekondari ,Wenyeviti wa Bodi pamoja na Maafisa Elimu Kata Manispaa ya Morogoro wametakiwa kusimamia elimu ili kufikia malengo ikiwa ni pamoja na kukuza ufaulu kwa kiwango cha daraja la kwanza, la pili na la tatu lakini pia kupunguza kiwango cha wanafunzi wanaofeli.
Wito huo umetolewa na Meya
Manispaa ya Morogoro Mhe. Khalid Matengo , wakati akizungumza katika
kikao kazi cha Tathmini ya matokeo ya Kitaifa ya mwaka 2025 kwa Shule za
Sekondari katika Ukumbi wa Bwalo Shule ya Sekondari Kilakala.
Meya Matengo , amesema
malengo ya Halmashauri katika upimaji wa kidato cha pili na kidato cha nne kwa
mwaka 2025 ni kufuta daraja sifuri na kuhakikisha kuwa kila mwanafunzi
anayemaliza kidato cha nne anapata cheti lakini pia kupunguza ufaulu wa daraja
la nne na kuongeza ufaulu bora yaani daraja I, II, na III.
Aidha,amesisitiza suala la
upatikanaji wa chakula Shuleni huku akiwataka Wazazi kutoa ushirikiano katika
hilo.
Pia, amewataka wazazi
kufuatilia mienendo ya watoto wakiwa shule na nyumbani ili kuongeza ufaulu .
Hata hivyo,amewataka walimu
kuwa wabunifu Zaidi kwa kutumia mbinu mbadala za kufundisha ili wanafunzi
waende na kazi ya walimu.
Mwisho,amezitaka shule zenye
maeneo makubwa kujikita Zaidi katika kilimo cha mboga ili kupata lishe bora kwa
wanafunzi.
Akiwasilisha taarifa ya matokeo
ya mtihani wa taifa wa kidato cha pili na kidato cha nne kwa mwaka 2025, Mkuu
wa Divisheni ya Elimu Sekondari, Sylevester Mwenekitete, amesema kuwa matokeo sio
mabaya kwa kwa wanafunzi wa kidato cha pili waliopimwa na kidato
cha nne hivyo ameomba jitihada za makusudi ziongezwe ili Manispaa katika
matokeo ya mwaka 2026 iwe ya Kwanza Kimkoa na Kitaifa.
Katika hatua nyingine,
Mwenekitete, amewapongeza wakuu wa shule ambao shule zao zimefanya vizuri na
kuwataka kuziendeleza jitihada hizo huku akiwataka wakuu wa shule ambazo
hazikufanya vizuri kuongeza jitihada ili wapate matokeo mazuri katika mitihani
inayofuata.
Mwenyekiti wa Kamati ya huduma
za Uchumi, Afya na Elimu Manispaa ya Morogoro, Mhe. Spear Komanya, amesema ili
ufaulu uongezeke lazima nidhamu kwa walimu na wanafunzi iimarishwe pamoja na
kuwajengea uwezo walimu kujifunza kwa wenzao waliofaulisha Zaidi.
Naye Afisa Elimu Mkoa wa Morogoro, Euphrasia
Buchuma, amewataka wakuu wa shule pamoja na Maafisa Elimu Kata kusimamia
nidhamu shuleni ikiwa ni pamoja na kuzuia utoro wa wanafunzi pamoja na walimu
ili kuinua taaluma kwani vitendo hivyo huathiri tendo la ufundishaji na ujifunzaji.
















Post a Comment