Header Ads

MACHINGA SHIUMA TAIFA WAPONGEZA UONGOZI WA SERIKALI MKOA WA MOROGORO KWA JITIHADA ZA KUWAJENGEA MAZINGIRA RAFIKI MACHINGA.


Viongozi wa SHIUMA Taifa , wakiwa pamoja na Viongozi wa SHIUMA Manispa ya Morogoro na machinga wakiwa katika picha ya pamoja.(wa sita kulia waliosimama mbele  Katibu wa SHIUMA Taifa, Ndg. Venatus Anatory). 

Mwenyekiti wa SHIUMA Taifa, Ernest Masanja, akizungumza na waandishi wa habari.

Mwenyekiti wa  Machinga Manispaa ya Morogoro   Juma Shaibu Ndeka,akizungumza na waandishi wa habari.

SHIRIKISHO la Umoja wa Machinga Taifa (SHIUMA) umeupongeza Uongozi wa Serikali ya Mkoa wa Morogoro kwa usimamizi mzuri na kuwajengea mazingira rafiki Machinga katika kufanya kazi zao za kuingiza kipato.

Kauli hiyo ya pongezi imetolewa leo Septemba 06/2021na Mwenyekiti wa SHIUMA Taifa  katika Mkutano wa waandishi wa habari na wamachinga uliofanyika Katika Ukumbi wa Mikutano wa Kingo Manispaa ya Morogoro Soko Kuu la Chifu Kingalu.

Akizungumza na Waandishi wa habari  kwa niaba ya  Wamachinga SHIUMA Taifa , Mwenyekiti wa Shirikisho hilo, Ndg. Ernest Masanja,   amesema Viongozi wa Mkoa wa Morogoro kwa kushirikiana na Viongozi wa Wilaya na Halmashauri wamefanya kazi kubwa katika kusimamia  utaratibu mzuri wa kuwapanga na kuwajengea machinga mazingira rafiki ya kufanya shughuli zao.

Amesema katika kipindi hiki cha karibuni, wameshuhudia mabadiliko makubwa sana hususani katika ujenzi wa mabanda ya Machinga  jambo ambalo limeonesha mwanga mkubwa na ukombozi wa machinga katika kufikia Tanzania ya Viwanda.

Amesema kuwepo kwa vibanda hivyo kutasaidia sana machinga kufanya kazi katika mazingira rafiki wakiwa na uhuru na kuweza kuitengenezea Serikali mapato na kusaidia  kuingizia Manispaa pato la ndani na kuacha kutegemea fedha za Ruzuku kutoka Serikali kuu.

Masanja, amechukua nafasi ya Kumpongeza  Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Albert Msando,  kwa kuwa karibu nao na kuwashirikisha  kwa kila jambo kitu ambacho kinawajengea faraja Wafanyabiashara na kuona Serikali inawaunga mkono kama alivyotamka Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwataka Wamachinga kufanya biashara zao bila ya kubugudhiwa.

"Mkuu wa Wilaya Kaka  yangu, Albert Msando, tunakushukuru sana pamoja na Uongozi wako wa Wilaya, umekuwa msaada mkubwa sana kwa upande wetu, umesimama mstari wa mbele kuhakikisha maslahi ya Wamachinga unayasimia kikamilifu, pia tumeona Manispaa inabadilika , miradi mikubwa mnayoitekeleza kwakweli inatupa faraja sana sisi wana Morogoro, kwani tunaamini baada ya kukamilika miradi hii Manispaa tutakuwa tuna vyanzo vizuri vya kukusanya mapato yetu ya ndani na kutengeneza miradi mingine kwa lengo la kuwahudumia Wananchi, nichukue nafasi hii kusema tunaomba usituchoke kaka yetu tunapopatwa na changamoto zidisha nguvu zako za kutukwamua" Amesema Masanja.

" Wale ambao watakwamisha mipango yetu  iwe Viongozi wa Serikali au viongozi wa machinga hatutakubali na jambo hilo tutaenda nalo hadi kwa Rais Samia , tunaomba Viongozi wa Halmashauri watushirikishe kwa kila jambo ambalo wanaona ina faa kufanyika kwani machinga wapo vizuri na wapo tayari kushirikiana na Serikali yao katika kufikisha gurudumu la maendeleo mbele" Ameongeza Aantory.

Naye Katibu wa SHIUMA Taifa, Ndg. Venatus Anatory, amewataka wafanya biashara mara baada ya zoezi kukamilika kuingia Sokoni basi wawe kitu kimoja kuhama na wala kusiwe na malalamiko na fujo za aiana yoyote.

" Serikali yenu imewatengenezea mazingira rafiki, mkafanye biashara sio kuzalisha majungu, fanyeni biashara zenu na wala msikiuke sheria , tupo hapa kuhakikisha zoezi la kuwaondoa katika mitaa ambayo Serikali ina matumizi nayo linafanikiwa kwa njia ya amani kabisa kwani Serikali bado ipo na sisi na inatupenda " Amesema Anatory.

Kwa upande wa Mwenyekiti wa  Machinga Manispaa ya Morogoro   Juma Shaibu Ndeka , amechukua nafasi hiyo kwa kumpongeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro, Ally Hamu Machela , huku akisema wapo tayari kumpa ushirikiano wakutosha kwani lengo lao sio kubaki nyuma ni kusonga mbele.

"Tunapenda kumkaribisha Mkurugenzi wetu katika Manispaa yetu, tunamhakikishia tutakuwa nae bega kwa bega na taarifa zozote atakazo zihitaji tutampatia lengo ni kuijenga Manispaa yetu isonge mbele na wamachinga wasonge mbele, tunamuomba kwa muda wake tuweze kuonana naye sisi viongozi na tuanze kumpatia maelezo juu ya Chama chetu, mikakati , mafanikio pamoja na changamoto ziazotukabili," Amesema Ndeka.

Katika mkutano huo na waandishi wa habari, Uongozi wa SHIUMA Taifa , umetoa zawadi ya vyeti vya shukrani kwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro , Mkuu wa Wilaya ya Morogoro  , Mstahiki meya Manispaa ya Morogoro pamoja na Mkurugezi Manispaa ya Morogoro kwa jitihada za kuwa mkombozi wa Machinga na kazi nzuri wanazozifanya.


No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.