Header Ads

DC NSEMWA AKABIDHI OFISI KWA DC KILAKALA ,AACHA UJUMBE KWA VIONGOZI

Aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Morogoro  ambaye kwa sasa ni Mkuu wa Wilaya ya Bahi,Mhe.Rebeca Nsemwa,  amekabidhi rasmi Ofisi  kwa Mkuu mpya wa Wilaya ya Morogoro Mhe.Mussa Kilakala.

Makabidhiano hayo ya Ofisi yamefanyika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya na kuwa na mkutano wa kuzungumza na watumishi wa Manispaa ya Morogoro Agosti 21-2024 kwenye Ukumbi wa Manispaa ya Morogoro.

DC Nsemwa, amewashukuru Viongozi wa Chama wa Wilaya na Mkoa, Viongozi wa Halmashauri za Manispaa ya Morogoro na Halmashauriya Wilaya ya Morogoro ,Madiwani wa Halmashauri zote , Kamati ya ulinzi na Usalama, Watumishi wa Wilaya hiyo na Viongozi wa Dini na Mila na Wananchi kwa Ushirikiano waliompa kipindi cha uongozi wake na kuwataka kushirikiana na Mkuu  mpya wa Wilaya hiyo ya Morogoro.

Aidha,DC Nsemwa,amemshukuru Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kumuamini katika utendaji 

Pia,amemuomba Mkuu wa Wilaya Mhe.Kilakala, kuhakikisha anafanikisha ndoto ya Manispaa kuwa Jiji  pamoja na kukabiliana na changamoto ambazo ni maji,miundombinu pamoja na suala la usafi japo tayari hatua zimechukuliwa za kuweka Mji safi.

"Kaka yangu Kilakala ni mzoefu sana ,mwadilifu na mchapakazi naombeni mumpe ushirikiano kama  mlivyonipa mimi, hakikisheni pia Viongozi mnaendelea kukemea vitendo vya ukatili wa kijinsia "Amesema DC Nsemwa.

Naye Mhe.Kilakala,ambaye ndiye Mkuu mpya wa Wilaya ya Morogoro, ametoa dira ya Wilaya kuwa itajikita katika ushirikiano wa kutatua changamoto zinazowakabili wananchi ili kuharakisha Maendeleo Wilayani humo ikiwemo usalama wa raia na mali zao, mahusiano kati ya Madiwani,watumishi na Mkurugenzi ambapo mahusiano hayo yatasaidia sana kufikia malengo na hatimaye ndoto ya Manispaa ya Kuwa Jiji inakamilika.

DC Kilakala, amewataka Watumishi kuchapa kazi  kwa bidii na kutoa wito kwa wananchi kuendelea kushirikiana na Serekali katika suala la maendeleo.

Aidha, DC Kilakala, amemshukuru Rais Dkt.  Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kumuamini  na kuahidi kumwakilisha vyema kwa kutatua changamoto za Wananchi na kusimamia shughuli za Maendeleo.

Kuhusu afya,DC Kilakala,amesema Mji wa Manispaa unapokea wageni wengi hivyo umakini unahitajika katika kutoa huduma ili kuepuka magonjwa ya milipuko pamoja na wajawazito na Wazee  kupewa vipaumbele katika vituo vya kutolea huduma za afya .

Kuhusu Wamachinga, amesema watashauriana namna bora ya kuhakikisha machinga wanakuwa salama na shughui zao na kuwataka Manispaa kusitisha operesheni za kamatakamata za machinga na wajasiriamali.

Amesema Fursa ya mradi wa SGR, kuna haja ya kuwa na Kituo cha Stop Center chenye huduma mbalimbali zitakazosaidia kuongeza mapato .

Mwisho,Mhe.Kilakala,amesema ipo  haja ya kuanzisha "MOROGORO SAMIA FESTIVAL"katika kupongeza juhudi za Rais Dkt.Samia za kuipatia Morogoro fedha nyingi za miradi ya Maendeleo.

Akizungumza kwa niaba ya Watumishi wa Manispaa, na Madiwani kwa ujumla, Meya Manispaa ya Morogoro, Mhe. Pascal Kihanga, amewapongeza Wakuu hao wa Wilaya kwa kuendelea kuaminika na kuteuliwa katika nyazifa hizo pia ametumia fursa hiyo kumkaribisha Mhe. Kilakala kuwa wamepokea maelekezo watashirikiana kikamilifu kuiletea Manispaa ya Morogoro Maendeleo.

No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.