Header Ads

MKURUGENZI MACHELA ATOA NENO BAADA YA MANISPAA YA MOROGORO KUIBUKA MSHINDI WA JUMLA MASHINDANO YA SHIMISEMITA



MKURUGENZI wa Manispaa ya Morogoro, Ally Machela, amewapongeza wanamichezo  watumishi wa Manispaa ya Morogoro walioshirki mashindano ya Shirikisho la Michezo Serikali za Mitaa Tanzania (SHIMISEMITA) kwa kuibuka washindi wa jumla wa michuano hiyo.

Pongezi hizo amezitoa leo  Novemba 2/2022  hafla fupi ya kukabidhi Makombe waliyoyapata katika Mashindano ya SHIMISEMITA.

Akizungumza mara baada ya kukabidhi makombe hayo, Machela, amewapongeza wanamichezo hao watumishi   kwa uwakilishi mzuri kwenye Mashindano ya  SHIMISEMITA ambapo Manispaa imefanya vizuri na kuwa washindi wa jumla mwaka 2022.

Machela ,amesema kuwa katika kuona Manispaa inaendelea kujiimarisha katika mashindano yajayo, amepanga kuwapa posho japo kidogo kwa wanamichezo hao  ili kuendelea kuwapa hali ya ushindani kwani  wameiheshimisha Manispaa katika nyanja za michezo.

"Napenda niwapongeze sana kamati nzima kuanzia walimu waliofanya maandalizi, wadau wetu, washangiliaji na waratibu wote lakini pongezi zangu za dhati kabisa ni kwa wanamichezo wenyewe waliotuletea vikombe hivi katika mashindano haya ambayo takribani miaka 8 hayajafanyika " Amesema Machela.

Naye Afisa Michezo Manispaa ya Morogoro, Asteria Mwang'ombe,amesema kuwa ushirikiano mkubwa baina ya walimu wa michezo, juhudi za wachezaji ndiyo siri kubwa ya mafanikio kwa Manispaa kuibuka mshindi wa jumla 

“Wakati wa kufanya uchaguzi wa wanamichezo tulikuwa na umakini mkubwa, tulifanya uchaguzi makini wa wanamichezo wetu, tuliwachagua kwa uwezo wao na siyo kwa upendeleo, tulicheza kwa tahadhari na kuheshimu wapinzani wetu katika michezo yetu yote, lengo likiwa ni kujenga timu imara na itakayotoa ushindani na kulinda hadhi ya Manispaa na hatimaye tukawa washindi wa jumla" Amesema Mwang'ombe.

Kwa upande wa  Mwenyekiti wa Mashindano kwa Watumishi Manispaa ya Morogoro, Neema Gwaseko,amesema ushindi walioupata umetokana na juhudi za wanamichezo hivyo matumaini yao ushindi huo watautafsiri kwenye michuano ijayo ambapo watakuwa na kibarua cha kutetea ubingwa wao.

"Tunawashukuru wanamichezo wetu walipambana sana, na ushindi ambao tumeupata  kamwe hawatabweteka na ushindi huo kwani mwakani tutaanza  maandalizi mapema ili kutetea ubingwa wetu" Amesema Gwaseko.

No comments

Theme images by A330Pilot. Powered by Blogger.